Kundi la vijana katika mji wa Garissa ulioko Kaskazini Mashariki mwa Kenya wameanza safari ya kutembea zaidi ya kilomita 700 kwa miguu kuelekea mji wa Mandera katika mpaka baina ya Kenya na Somalia ilikuchochea amani.
Vijana hao wa asili ya kisomali wanalenga kuhubiri amani na kuchochea wenyeji wa eneo hilo lililoshuhudia mashambulizi mengi kutoka kwa kundi la wapiganaji wa kiislamu la Al Shaabab.
Mwezi April wanafunzi takriban 150 wa chuo kikuu cha Garissa waliuawa katika shambulizi baya zaidi kuwahi kutekelezwa nchini kenya na kupelekea chuo hicho kufungwa.
Aidha waalimu na wafanyikazi wa umma kutoka maeneo mengine ya Kenya wametoroka kutoka eneo hilo la Garissa , Wajir na Mandera wakihofia usalama wao kufuatia mashambulizi yanayowalenga.
Shule nyingi za umma na hospitali zimeathirika pakubwa kutokana na kuhama kwao.
Vijana hao sasa wanalenga kuwahakikishia wenyeji na wageni kuwa eneo hilo lina matumaini ya kurejea kwa amani ya kudumu na mtagusano baina ya wenyeji na wageni.
Vijana hao wanalenga kukamilisha sfari hiyo katika kipindi cha siku 25 zijazo.
BBC SWAHILI.