
Siku Moja baada ya kujiuzulu kwa Mwanasheria mkuu Jaji Fredrick Werema, Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka kwa mara nyingine amejitokeza hadharani na kutoa msimamo wake kwamba hana sababu ya kujiuzulu kwenye nafasi yake kwa kuwa hakuhusika kwa namna yeyote kwenye sakata la uchotwaji wa mabilioni kwenye akaunti ya Escrow. Akizungumza na waandishi wa habari asubuhi leo jijini Dar es Salaam, Profesa Tibaijuka amesema kuwa pamoja na kuwepo kwa shinikizo la kutaka kujiuzulu, yeye binafsi ameona hana sababu ya kufanya hivyo kwani kufanya hivyo ni kukubali kuwa amehusika moja kwa moja kwenye kashfa hiyo jambo ambalo si la kweli. Profesa Tibaijuka amekwenda mbali zaidi na kusema kuwa uvumi unaoendelea kusambazwa mitaani ni ishara mbaya kwani unawaaminisha wananchi kuwa amehusika katika sakata hilo wakati yeye hajahusika na jambo lolote. “Huu uvumi unatakiwa kuachwa, sioni sababu yeyote ya mimi kujiuzulu kwa kuwa sijahusika kwa namna yeyote kwenye sakata hili la Escrow” anasema Profesa Anna Tibaijuka.