PROFESA APENDEKEZA MASKINI WAGAWANE WAKE NCHINI CHINA.

By | 12:53


China
Image copyrightAP
Image captionWavulana huwa wengi kuliko wasichana nchini Uchina
Profesa mmoja nchini Uchina amezua mjadala mkali baada yake kupendekeza kwamba wanaume maskini wawe wakigawana wake.
Pendekezo lake anadai litasaidia kusuluhisha tatizo linalotokana na uhaba wa wanawake nchini humo.
Wazo hilo la Xie Zuoshi, ambaye ni profesa wa kiuchumi katika Chuo Kikuu cha Zhejiang, limeshutumiwa na wengi wanaosema linakiuka maadili ya jami.
Uchina ni moja ya mataifa yenye tofauti kubwa sana ya idadi ya watu wa jinsia zote mbili, kukiwa na wavulana 118 kwa kila wasichana 100.
Hii ina maana kwamba mwishowe, kuna wavulana ambao huwa hawana msichana wa kuoa.
Pengo hilo kubwa sana husababishwa na sera ya Uchina iliyotaka familia ziwe zikizaa mtoto mmoja pekee. Watoto wavulana pia hupendelewa sana kwa sababu za kitamaduni.
Katika ulimwengu wa sasa, wanawake wengi pia wamekuwa wakihamia mijini kutafuta kazi na kuwaacha wanaume mashambani wakiwa hawana wanawake wa kuoa.
Kwenye pendekezo lake lililonukuliwa sana na vyombo vya habari nchini Uchina, Prof Xie alisema kuna ripoti kuwa huenda Uchina ikawa na makapera kati ya 30 milioni na 40 milioni ifikapo mwaka 2020.
Hitaji kubwa la wanawake na uhaba wao limesababisha “thamani ya wanawake kwenda juu”, aliandika.
"Wanaume wa pato la chini watafanya nini? Njia moja ni wanaume kuungana na kwa pamoja watafute mke. Hili si wazo la ajabu. Katika baadhi ya maeneo ya mashambani yenye watu maskini kuna visa vya ndugu kuungana na kuoa mke mmoja, na wanaweza kuishi raha mustarehe.”
ChinaImage copyrightSina
Image captionXie alitoa mapendekezo yake kwenye makala aliyoipa kichwa 'Makapera milioni 30'
Kadhalika amependekeza kuwepo na ukuaji wa kiuchumi ambao utawawezesha makapera maskini kupata pesa zaidi na hivyo kuvutia wanawake kutoka maeneo mengine kama vile kusini mashariki mwa bara Asia au hata Afrika.
Uhaba wa wanawake katika baadhi ya maeneo ya Uchina kumepelekea wanaume wengi kuoa wanawake kutoka nchi jirani kama vile Vietnam na Myanmar (Burma). Kadhalika, umesababisha ongezeko la ulanguzi wa watu na watu kutapeliwa pia kupitia ndoa.
Mfano ni kisa ambapo wanawake karibu 100 kutoka Vietnam, waliokuwa wameozwa kwa wanaume wa Kichina, walitoweka ghafla. Wanaume hao walikuwa wamelipa $18,600 kuwapata wanawake hao.
Newer Post Older Post Home