ASKARI WA WANYAMAPORI WATUHUMIWA KUWAPIGA RAIA.

By | 06:14

                                
Mbeya.
Baadhi ya wafugaji wa vijiji vinavyozunguka Hifadhi ya Ruaha wilayani hapa Mkoa wa Mbeya, wamedai kupigwa na askari wa wanyamapori na kuwatoza kiwango kikubwa cha fedha kwa kosa la mifugo yao kuingia kwenye maeneo ya hifadhi hiyo.
 
Wakizungumza na waandishi wa habari wilayani hapo, wafugaji hao, walidai kuwa imekuwa kawaida kwa askari hao kukamata mifugo na kuwatoza faini kubwa na wakati mwingine kuwashambulia kwa vipigo.
 
Mmoja wa wafugaji hao,  Igembe Mahola, Mkazi wa Kijiji cha Iyala, alidai hivi karibuni ng’ombe wake 143 walikamatwa na askari hao wa wanyamapori wakidaiwa kukutwa ndani ya hifadhi na alipofuatilia, alishushiwa kipigo kisha kutozwa faini ya Sh.  milioni 9.
 
Mahola alidai kuwa kwenye stakabadhi yake, aliandikiwa kuwa amelipa faini ya Sh. milioni 5 badala ya Sh. milioni 9 alizoamriwa kulipa na askari hao.
 
Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wafugaji Wilaya ya Mbarali, Makeresia Pawa, alisema  askari hao wanatumia udhaifu wa serikali juu ya migogoro ya mipaka iliyopo kujinufaisha.
 
Pawa alisema mara kadhaa imeripotiwa na wafugaji kuwa askari hao huswaga ng’ombe ndani ya hifadhi baada ya kuwakuta wakiwa katika maeneo ya jirani ili kujipatia fedha.
 
“Tumepaza sana sauti zetu sisi wafugaji na inaonekana serikali imekuwa ngumu kutuelewa katika hili hivyo basi tunaiomba kutusikiliza kilio hiki vinginevyo tutakuja na maazimio magumu sana, ”alisema Pawa.
 
Akijibu malalamiko hayo,  Mkuu wa Hifadhi ya Ruaha,  Christopher Timbuka,  alisema hajayapata ila anachofahamu askari hao kuendelea kutekeleza wajibu wao ili kuhakikisha hakuna mifugo inayoingia ndani ya hifadhi hiyo ili kutunza mazingira.
 
Timbuka alisema madai ya kutozwa faini kubwa na kupewa stakabadhi zenye viwango pungufu, amekuwa akiyasikia,  lakini wafugaji wameshindwa kutoa ushirikiano kwa kuwataja majina askari wanaojihusisha na  vitendo hivyo ili hatua zichukuliwe. 
 
Ametoa wito kwa wafugaji hao waache kupeleka  mifugo yao ndani ya hifadhi hiyo ili kuepukana na adha hizo wanazokutana nazo baada ya kukamatwa. 
CHANZO: NIPASHE
Newer Post Older Post Home