LOWASSA:NINA UHAKIKA WA USHINDI ASILIMIA 80.

By | 23:28


Mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa.
Mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, amesema ana uhakika wa kushinda kwa asilimia 80 na kwamba atakuwa rais wa mabadiliko na siyo maneno.
 
Aliyasema hayo jana kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika katika uwanja wa Kigoda CCM Handeni mkoani Tanga.
“Kuna watu wanasema nitapita kwa silimia 50 au 60 hivi, kwa hali niliyoiona vijijini na mijini, naona nitapata asilimia 80, naomba mfanye nipate hiyo, nitakuwa rais siyo rais wa maneno ni rais wa mabadiliko.
 
“Nimeongoza haya mabadiliko kwa heshima, nataka niongoze taifa hili wajue tunaweza kuwa bora kuliko mataifa mengi, tuachane na umaskini, nauchukia sana umaskini,” alisema Lowassa.
 
Alisema kwa sasa polisi wanawakamata ovyo vijana wanaoonyesha mapenzi kwa Chadema, jambo alilosema linaweza kusababisha vurugu nchini.
 
“Nimeona jana Tanga na maeneo mengine tabia inayoanza ya kukamata vijana wa Chadema, nawaambia serikali  waache, wanachochea fujo, vijana hawa ukiwachokoza utaanzisha fujo. Sisi tuna hakika ya kushinda asubuhi kweupeee, kwa hiyo hatuna sababu ya kufanya fujo na waache vitisho vya silaha na bunduki barabarani, ni kutisha nchi,” alisema Lowassa.
 
Ili kuhalalisha ushindi wake huo, aliwataka wafuasi wake kumpigia kura kwa wingi ili hata kama baadhi zitaibiwa,  ashinde.
 
“Tumechoka na miaka 54 ya CCM, Tanzania bila CCM inawezekana, tuonyeshe kazi,” alisema Lowassa.
 
Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, akizungumzia suala la polisi, alisema vijana wanaobeba bendera za Chadema wakionekana wakiwa wamefuatana hata kama ni watatu, wanakamatwa lakini wanaobeba bendera za CCM hata wakiwa wengi kiasi gani, hawaguswi.
 
CHANZO: NIPASHE
Newer Post Older Post Home