Manchester, England. Timu hasimu za jiji la Manchester, United na Manchester City zimeshindwa kutambiana baada ya kulazimishana sare ya 0-0 katika mchezo wa jana wa Ligi Kuu England.
Man United ilikuwa na mchezo mzuri na kuutawala kwa kiasi kikubwa mchezo huo, lakini ilishindwa kutumia faida hiyo ya kucheza nyumbani kuifunga Man City iliyonekana kumkosa mshambuliaji wao hatari, Sergio Aguero aliye majeruhi.
Kwa matokeo hayo, Man City imerudi kileleni mwa Ligi Kuu Englandkwa tofauti ya mabao dhidi ya Arsenal iliyoongoza kwa muda baada ya ushindi wao wa juzi wa mabao 2-1 dhidi ya Everton.
Katika michezo mingine iliyochezwa jana, Tottenham au Spurs iliinyuka Bournemouth kwa mabao 5-1, wakati Sunderland ikiibuka na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Newcastle.
Mechi nyingine ilikuwa baina ya Liverpool na Southampton zilizokuwa zikicheza jana usiku.